NEW UPDATES

SALAMU ZA IGP SIRRO KWA WANAO ENDESHA MAUAJI KIBITI.

4 hrs ago  Kitaifa

Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali Simon Sirro, amesema watu wanaotumwa kutekeleza mauaji Wilaya za Kibiti, Mkuranga na Rufiji, ambao wanaua raia na askari watajibiwa kwa ubaya na kwamba wametangaza vita dhidi yao.

“Sisi Tanzania hatujazoea vurugu za namna ile kwa hiyo wale ambao walikuwa wametumwa walifikiria Tanzania kama nchi nyingine wataona majibu yake,” alisema na kuongeza kuwa: “Tangu zamani sisi ni wamoja na tunapendana kwa hiyo wale waliokuwa wametumwa vibaya vibaya na sisi tutawajibu kwa ubaya ubaya tu.”

Amesisitiza kuwa suala la ulinzi ni la watu wote na kwamba wananchi wa maeneo hayo wanapaswa kujilinda kwa kuanzisha vikundi vya ulinzi shirikishi. Amesema Jeshi la Polisi linakwenda vizuri na suala la mauaji ya Kibiti na kwamba muda si mrefu kutakuwa na majibu mazuri.

“Maeneo hayapitiki, Kibiti, Ikwiriri, Mkuranga hata maeneo mengine ya nchi wananchi wanapaswa kujilinda kwa kuanzisha ulinzi shirikishi,” alisema IGP Sirro.

Baadhi ya watuhumiwa wanaoendesha vitendo vya mauaji mkoani Pwani kwa mujibu wa Jeshi la Polisi ni pamoja na Abdulshakur Ngande Makeo, Faraj Ismail Nangalava, Anaf Rashid Kapera, Said Ngunde, Omary Abdallah Matimbwa, Shaban Kinyangulia, Haji Ulatule, Hassan Uponda, Rashid Salim Mtulula, Hassan Nasri Mzuzuri na Hassan Njame.

No comments

https://instagram.com/bakihotnews?utm_medium=copy_link