NEW UPDATES

DAR- MKAGUZI WA VYETI FEKI ATAJWA KWENYE ORODHA YA WENYE VYETI FEKI.

DAR ES SALAAM.

DAR ES SALAAM: Kuna msemo unaosema kuwa muosha, huoshwa. Huo ndio unaweza kuelezea kilichotokea katika Halmashauri ya Manispaa ya Temeke baada ya mkaguzi mmoja aliyekuwa akifanya uhakiki wa vyeti feki kutajwa miongoni mwa watumishi wanaotuhumiwa kuwa na vyeti vya kughushi.

Hatua hiyo hiyo imekuja baada ya kukamilika kwa mafanikio makubwa zoezi la uhakiki wenye vyeti feki katika maeneo mbalimbali nchini.

Mkaguzi huyo aliyetajwa kwa jina la Adolph Shayo, jina lake ni namba 1,023 katika orodha ya watumishi 9,932 wenye vyeti aliyokabidhiwa Rais Dkt Magufuli Aprili 28 mwaka huu mjini Dodoma.

Wakati wa ukaguzi, Shayo alijipatia sifa ya kuwa mkali na msumbufu akidaiwa kuwataka mara kwa mara watumishi wenzake kumpelekea vyeti vyao.

Mmoja wa watumishi waliokaguliwa vyeti vyao na Shayo alisema kuwa walimu walipata shida wakati wa uhakiki sababu alikuwa chini ya Shayo. Alisema kuwa alishangaa kusikia ametajwa miongoni mwa wenye vyeti feki wakati yeye ndiye aliyekuwa akihakiki.

Mkurugenzi wa Manispaa ya Temeke, Nassib Mmbaga alisema kuwa, baada ya uhakiki ilibainika kuwa vyeti vyake vilikuwa na kasoro (ambayo hawakuitaja) na walipomtaka Shayo kuthibitisha, hakufanya hivyo.

Shayo alikuwa ni Mtumishi katika Halmashauri ya Manispaa ya Temeke akifanya kazi kwenye Idara ya Elimu na Msaidizi Kitengo cha Bohari ya Manispaa lakini lilipokuja suala la uhakiki vyeti ilibidi afanye kazi kama msaidizi.

“Hata kama ni mkaguzi lazima akaguliwe. Hata mimi (Mkurugenzi) nilikaguliwa. Lakini tulipokagua vyeti vyake (Shayo), tuligundua vina shida,” alisema Mkurugenzi huyo.

Licha ya kuwa Shayo hakuthibitisha uhalali wa vyeti vyake kama alivyotakiwa, hata hajatuma barua ya kukata rufaa licha ya mkurugenzi kusema hadi sasa wamepokea barua za rufaa 60.

No comments

https://instagram.com/bakihotnews?utm_medium=copy_link