NEW UPDATES

FAHANU MBINU MPENZI WAKO ANAZOWEZA KUTUMIA KUCHEPUKA KWA URAHISI.

Mahusiano

Kwa hali ilivyo sasa imefika mahali inabidi mtu ajiulize kuna tatizo gani katika suala la wanaume kuchepuka, kwani kadiri siku zinavyozidi kwenda suala hili linarahisishwa na kuonekana kama jambo la kawaida kwenye jamii.

Hali imezidi kuwa mbaya sababu hata wale waliokuwa wakionekana kuwa ni waaminifu, lakini nao sasa wakipata nafasi hiyo hawasubiri wala kujiuliza mara mbili.

Sakata hili kadiri linavyozidi kushika mizizi kwenye jamii ndivyo hivyo hivyo na mbinu mpya za uchepukaji huibuka kila iitwapo leo. Jaribu kufikiri, mke au mumeo anakuaga alfajiri anatoka kwenda ofisi ili awahi ofisini kabla msongamano wa magari haujawa mkubwa, kwa mtu muelewa hiyo ni sababu ya msingi, lakini kumbe haelekei ofisini moja kwa moja, anapitia sehemu kuonana na mchepuko wake kisha ndio safari ya ofisini ianze.

Wakati mwingine kuchepuka kumerahisishwa hadi unajiuliza kwanini kuna wanyama wanaweza kuwa na uhusiano na mnyama mmoja tu hadi kifo lakini kwa binadamu mwenye akili ya kupambanua mambo anashindwa?

Dini inasisitiza kuwa mwaminifu, kuwa na mpenzi mmoja, lakini kila mara elimu juu ya zinaa hutolewa na athari zake kuwekwa hadharani, lakini wanaume kwa wanawake hakuna anayejali hilo.

Lakini tabia hii ya kuchepuka imerahisishwa zaidi na teknolojia ambapo watu wengi hukutana mitandaoni, kubadilishana namba, kutumiana picha na vitu vingine na mwisho wa siku anakuwa mchepuko wake.

Kuna baadhi ya watu husema kuwa mwanamke akichepuka sio jambo la bahati mbaya kama inavyokuwa kwa mwanaume, kwake yeye anakuwa tayari ameshapanga kwamba angechepuka.

Suala baya kuhusu mitandao ya kijamii ni kuwa imesababisha ndoa na mahusiano ya watu wengi kuvunjika kwani mtu akichepuka anaamini kuwa ataweza kufanya siri lakini mwisho wa siku anapatikana na ushahidi ambapo upande wa pili unakuwa mgumu kurudisha moyo nyuma.

Mbinu nyingine inayotumiwa kuchepuka ni kubadilisha majina kwenye simu na kuayahifadhi (save) kwa kutumia majina ya uongo. Mume anaweza kuandika jina la mchepuko wake, Juma, akipiga mke wake anakuwa hana wasiwasi kwa sababu anajua ni Juma anapiga kumbe upande wa pili ni Halima au Grace.

Mwanamke au mwanaume ambaye ‘inbox’ au ‘sent items’ kwenye simu yake mara nyingi huwa haina jumbe, ni wa kutiliwa shaka kwani lazima kuna jambo anaficha. Lakini pia ambaye ‘Call log’ yake inakuwa haina kumbukumbu ya simu zilizopigwa au kupokea, hapo pia kuna tatizo.

Teknolojia inavyokuwa, dunia inazidi kuwa ndogo, urahisi wa kuchepuka unaongezeka lakini na mbinu za kumkamata anayechepuka nazo zinaongezeka, fanya maamuzi sasa kuchepuka au kuwa mwaminifu.

No comments

https://instagram.com/bakihotnews?utm_medium=copy_link