NEW UPDATES

NSSF YATANGAZA NAFASI ZA KAZI KUZIBA MAPENGO YA WALIOTUMBULIWA.

NSSF YATANGAZA NAFASI ZA KAZI KUZIBA MAPENGO YA WALIOTUMBULIWA

Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF) limetangaza nafasi za kazi zilizoachwa wazi na vigogo 12 waliotumbuliwa kwa tuhuma mbalimbali. Kati ya vigogo hao 12, vigogo sita walikuwa wanatumikia nyadhifa za juu kabisa za utendaji ndani ya shirika hilo.

Tangazo la nafasi za kazi lililotolewa jana na shirika hilo limeorodhesha nafasi 13 ambazo zinatakiwa kujazwa.

Katika nafasi hizo 13, nafasi saba ni wakurugenzi ambazo ni:

Mkurugenzi wa Mipango, Uwekezaji na Miradi (iliyokuwa inashikiliwa na Yacoub Kidula),

Mkurugenzi wa Rasilimali Watu na Utawala (iliyokuwa inashikiliwa na Chiku Matessa),

Mkurugenzi wa Fedha (iliyokuwa inashikiliwa na Ludovick Mrosso),

Mkurugenzi wa Udhibiti Majanga (iliyokuwa inashikiliwa na Sadi Shamliwa),

Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Hesabu za Ndani (iliyokuwa inashikiliwa na Pauline Mtunda),

Mkurugenzi wa Uendeshaji (iliyokuwa inashikiliwa na Crescentius Magori) na

Mkurugenzi wa Tehama.

Pia zipo nafasi nne ambazo ni Ofisa Masoko na Uhusiano, Meneja Usalama, Meneja wa Mipango na Uwekezaji na Meneja Miradi. Nafasi nyingine ni Makatibu Muhtasi 12 na Madereva 15.

Tangazo hilo limekuja ikiwa ni takribani miezi 11 kupita tangu Bodi ya Udhamini ya shirika hilo kuwasimamisha kazi vigogo hao kwa tuhuma za ubadhirifu wa fedha za umma, matumizi mabaya ya ofisi, kukiuka sheria na kanuni za usimamizi wa miradi na manunuzi.

Katika azimio la Bodi ya Udhamini ya shirika hilo la kuwasimamisha kazi watumishi hao, ukiachia mbali Wakurugenzi sita, pia mameneja watano na mhasibu mmoja walisimamishwa ili kupisha uchunguzi. Mameneja waliosimamishwa kazi ni Amina Abdallah (Meneja Utawala), Abdallah Mseli (Meneja Uwekezaji), Mhandisi John Msemo (Meneja wa Miradi), Chedrick Komba (Meneja Kiongozi –Mkoa wa ki-NSSF wa Temeke), Mhandisi John Ndazi (Meneja Miradi) pamoja na Mhasibu Mkuu wa Shirika hilo, Davis Kalanje.

No comments

https://instagram.com/bakihotnews?utm_medium=copy_link