NEW UPDATES

MAMBO MUHIMU SANA UNAYOPASWA KUJUA KUHUSU HISA ZA VODACOM

29 mins ago  Makala

Habari rafiki?

Nimeandaa mwongozo huu mfupi kuhusu UWEKEZAJI KWENYE HISA na HISA ZA VODACOM ili ukusaidie wewe kama rafiki yangu kuweza kufanya maamuzi sahihi. Nimekuwa naona wengi wakishindwa kufanya maamuzi au wakipotoshwa, naamini kupitia mwongozo huu, utaongeza maarifa yako na kuweza kufanya maamuzi sahihi.

Kabla sijaingia kwenye mwongozo huu, naomba niweke wazi ya kwamba;

1.      Ushauri ninaotoa hapa ni kwa uelewa na uzoefu wangu kama mwekezaji.

2.      Sina uhusiano wowote na vodacom na wala silipwi kwa kuandika haya.

3.      Nimeshanunua hisa za vodacom katika soko hili la awali.

Hivyo rafiki soma, na fanya maamuzi sahihi ukiwa na taarifa sahihi kwako.

Karibu sana;

SEHEMU YA KWANZA; MAANA YA UWEKEZAJI KWENYE HISA.

Uwekezaji kwenye hisa ni fursa ya mtu kuwa sehemu ya wamiliki wa biashara au kampuni husika.

Kwa mfano kama unataka kuanzisha biashara ya mtaji wa laki moja, na wewe una elfu 10 tu, unaweza kuwatafuta watu 9 kila mtu akachangia elfu 10 na jumla mkapata laki moja.

Hivyo kama biashara itapata faida, kila aliyechangia atapata sehemu ya faida hiyo.

Na kama biashara itapata hasara, basi inakuwa hasara kwa kila mtu.

Uwekezaji wa hisa ndiyo uko hivyo, ila hapa ni kwa kiwango kikubwa na udhibiti mkubwa wa kisheria.

Unaponunua hisa za kampuni, maana yake unakuwa umechangia mtaji wa kampuni na hivyo kuwa mmoja wa wamiliki.

Lakini wewe huhusiki kwa namna yoyote ile kwenye uendeshaji wa kampuni.

Kampuni itaendeshwa kulingana na taratibu zake.

Faida inapopatikana, basi unapewa gawio kama mwanahisa, kulingana na hisa ulizonazo.

Faida za kuwekeza kwenye hisa.

Zipo faida nyingi sana za kuwekeza kwenye hisa, hizi hapa ni chache.

1. Kupata faida kutokana na fedha ulizowekeza. Hapa fedha yako inafanya kazi huku wewe ukiwa unaendelea na mambo yako mengine.

Na hapa ndipo dhana halisi ya utajiri ilipo, PALE FEDHA INAKUFANYIA WEWE KAZI badala ya wewe kuifanyia kazi fedha ambao ni umasikini.

2. Kupata ongezeko la thamani ya fedha uliyowekeza. Licha ya gawio la faida, hisa huweza kuongezeka thamani, kulingana na uimara wa uchumi na soko. Kwa mfano unaweza kununua hisa ikiwa shilingi 500, baada ya muda thamani yake ikawa sh 1000, hapo ukiuza unauza kwa bei ya wakati huo siyo ile uliyonunulia.

3. Ni sehemu ya kuweka fedha ambayo huwezi kuitoa haraka.

Watu wengi wamekuwa wakilalamika kushindwa kuzituliza fedha, wakiweka benki hawawezi kujizuia kwenda kuzitoa. Unapowekeza kwenye hisa siyo rahisi kupata fedha zako kama unavyoenda kutoa kwenye atm, inabidi ujaze fomu kuuza hisa na usubiri zinunuliwe.

Hasara za kuwekeza kwenye hisa.

Hisa siyo kitu chenye faida tu wakati wote, zipo hasara na hatari pia. Zifuatazo ni baadhi kati ya nyingi.

1. Kampuni ikipata hasara na wewe unapata hasara. Kampuni ikifilisika na wewe unapoteza kabisa kile ulichowekeza.

2. Mabadiliko ya kiuchumi kama mfumuko wa bei vinaweza kuathiri thamani ya hisa, badala ya kupanda bei zinashuka bei.

3. Mabadiliko ya kisiasa yanaathiri pia soko la hisa.

4. Huna udhibiti wa moja kwa moja wa fedha zako, unanunua hisa lakini wanaoongoza kampuni ni wengine, hivyo wakifanya makosa yatakugharimu na huna namna ya kuokoa hilo, hata kama una ujanja kiasi gani.

SEHEMU YA PILI; HISA ZA KAMPUNI YA VODACOM.

Vodacom Tanzania imeweka sokoni hisa 560 000 100 kwa bei ya shilingi 850 kwa kila hisa.

Kwa sasa hisa hizi zinauzwa kwenye soko la awali mpaka tarehe 11/05/2017, baada ya hapo hisa zitaandikishwa kwenye soko la hisa la dar es salaam (DSE)

Kila mtu anayetaka anaweza kununua hisa hizi,

Kiwango cha chini cha kununua ni hisa 100.

Unaweza kununua hisa kupitia madalali wa soko la hisa, bank mbalimbali zilizoteuliwa kama nbc, wakala wa max malipo na hata njia ya simu.

Hii ni fursa ya uwekezaji iliyo wazi kwa kila Mtanzania.

Uimara au faida za hisa za vodacom;

1. Vodacom ndiyo mtandao wenye watumiaji wengi tanzania, hivyo kuwa na soko kubwa la huduma zake.

2. Huduma za data zinakua kwa kasi kutokana na ongezeko la watu wanaotumia mtandao wa intaneti.

3. Huduma ya M Pesa imeendelea kuwa tegemeo kwa watanzania wengi ambao hawawezi kufikia benki na hata kwenye miamala ya kibiashara.

4. Kampuni imeonesha ukuaji wa kuridhisha tangu kuanzishwa kwake hapa nchini mwaka 1999 mpaka sasa.

5. Udhibiti wa kisheria ulipo chini ya mamlaka ya masoko ya mitaji na soko la hisa la dar es salaam.

Hatari au hasara inayoweza kutokana na hisa za Vodacom.

Zipo hatari zinazoweza kusababisha hasara kwa wale watakaowekeza kwenye hisa za vodacom, hizi ni baadhi kati ya nyingi;

1. Ushindani mkali wa kibiashara kwenye sekta ya mawasiliano. Ipo mitandao yenye nguvu na mingine inakua kwa kasi, kama tigo, airtel na halotel.

2. Mazingira magumu ya kibiashara hapa nchini. Vodacom ina baadhi ya kesi za kibiashara zinazotokana na sheria mbalimbali za kibiashara nchini, kama sheria ngumu ya kodi.

3. Miundombinu isiyo ya uhakika, inayoweza kupelekea gharama za uendeshaji kuwa kubwa na hivyo faida kuwa kidogo. Mfano kukosekana kwa umeme wa uhakika.

4. Kesi mbalimbali za kibiashara zinazoweza kutokana na shughuli za kampuni.

5. Mabadiliko ya sera na sheria za nchi yanayoweza kubadili uendeshaji wa makampuni na huduma mbalimbali.

6. Kupata hasara au kufa kwa kampuni, kwa sababu zozote za kibiashara.

SEHEMU YA TATU; USHAURI WANGU KWAKO KUHUSU HISA HIZI.

Kwa wale ambao wanapenda kuwa wawekezaji wa muda mrefu, basi unaweza kuanza kwa kuwekeza kwenye hisa hizi za vodacom. Japokuwa hakuna yeyote anayeweza kutabiri kwa uhakika hisa hizi zitafanya vipo zikishaingia sokoni, kwa mipango ya muda mrefu, mwekezaji hawezi kupoteza.

Kama unataka kununua kwa sababu unafikiri zikiingia sokoni bei itapanda ghafla na hivyo utapiga hela, nikukatishe tamaa kwamba unafanya kitu hatari, utapata hasara na kusema uwekezaji siyo mzuri.

Mwisho kabisa wekeza fedha ambayo ilikuwa ni ya akiba tu, au upo tayari kuipoteza. Usitoe fedha kwenye biashara ambayo inakuzalishia kwa ajili ya kwenda kununua hisa. Na usijaribu kabisa kuchukua mkopo kwa ajili ya kwenda kununua hisa. Chukua sehemu ya akiba yako na nunua hisa. Kama huna kwa sasa usiumie, hisa hizi zitaingia kwenye soko la hisa na jipange utaweza kuzinunua wakati mwigine.

Kama una akiba kiasi kikubwa na hujui kiasi gani uwekeze, nakushauri uwekeze asilimia kumi ya akiba uliyonayo sasa. Ni sehemu nzuri kuanzia na kadiri unavyojifunza utaendelea kuwekeza zaidi.

Nimepata taarifa pia kwamba kwa watumishi wa serikali, wamepewa nafasi ya kununua hisa kupitia fedha zao zilizopo kwenye mifuko ya kijamii. Hii ni fursa nzuri kwa watumishi kuitumia. Kama una fedha huko chukua asilimia kumi na nunua hisa. Kwa sababu kwa vyovyote vile huwezi kuzipata fedha hizo kwa haraka, hivyo kuzihamishia kwenye hisa itakuwezesha kunufaika zaidi pale hisa zinapofanya vizuri.

Na mwisho kabisa, wale wanaohusisha uwekezaji huu na siasa, hasa kwa sababu viongozi wa serikali wanasisitiza watu wanunue, nawashauri wajifunze zaidi kuhusu uwekezaji. Uendeshaji wa kampuni na masoko haya ya mitaji una sheria na taratibu zake. Zielewe na wekeza huku pia ukijua unaweza kupoteza.

Naamini umepata mwanga kidogo kuhusu hisa na hisa za vodacom. Kama una swali karibu uulize hapo chini na nitakujibu kadiri ya uelewa wangu.

Rafiki na Kocha wako,

Makirita Amani

No comments

https://instagram.com/bakihotnews?utm_medium=copy_link