NEW UPDATES

TRA yabadili mfumo matumizi ya EFDs


IMEANDIKWA NA KATUMA MASAMBAIMECHAPISHWA: 14 APRILI 2017
Kaimu Kamishna Mkuu wa TRA, Neema Mrema
MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) imefanya mabadiliko katika mfumo wa usimamizi wa matumizi ya Mashine za kielektroniki za Utoaji risiti (EFDMS) ili kudhibiti uwezekano wa kughushi risiti.
Aidha, mfumo huo una usalama wa hali ya juu, kwani miamala na risiti zote zitakuwa na saini ya kielektroniki na “QR Code”, hivyo kupunguza uwezekano wa kughushi risiti kutoka kwenye mashine za kielektroniki ambazo hazijasajiliwa na mfumo wa mamlaka hiyo.
Akizungumza wakati wa kufungua semina ya Walipakodi Wakubwa, Kaimu Kamishna Mkuu wa TRA, Neema Mrema alisema mfumo huo ni wa kiintelijensia kwani una uwezo wa kutambua hati ya mauzo kwa mkopo, marejesho ya mauzo, risiti halali na durufu.
“Mfumo umezingatia kupunguza gharama, kwani mfumo huu ni wa Tehama ambao utaipunguzia gharama serikali kununua mashine halisi kwa kuwa umeunganishwa na seva ya TRA,” alisema Neema.
Alisema mfumo huo pia una ufanisi mkubwa na ni rafiki kwani unaweza kuunganishwa na mifumo mingine kama mifumo ya ankara, mauzo na stakabadhi mbalimbali kwa kufanya mabadiliko machache, pia unaruhusu matumizi ya fedha mbalimbali.
Semina hiyo ya siku moja imewakutanisha walipakodi wakubwa kwa ajili ya kupata elimu juu ya Sheria ya fedha ya mwaka 2016 na Sheria ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) ya mwaka 2014.
Mada zingine zilizowasilishwa ni kodi ya zuio katika bidhaa na huduma, mfumo wa ukusanyaji wa maduhuli kwa kutumia mashine za kielektroniki za utoaji risiti (vitual EFD).
Akizungumzia kodi ya zuio, Neema alisema utekelezaji wa Kodi ya zuio iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2013 umekuwa na changamoto mbalimbali kwa idara na taasisi za serikali.

No comments

https://instagram.com/bakihotnews?utm_medium=copy_link